Tarehe 11 Machi, 2026 Mjini Beira Jimbo la Sofala, Msumbiji, kilifanyika kikao baina ya Gavana wa Jimbo la Sofala, Mhe Lourenço Bulha na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Msumbiji Mhe. CP. Hamad Khamis Hamad, kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na ushirikiano wa kiuchumi kati ya pande hizo mbili, hususan katika sekta ya usafirishaji wa baharini na maendeleo ya bandari.
Viongozi hao walijadili umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya Bandari ya Beira na bandari za Tanzania ili kuongeza ufanisi wa biashara ya kikanda, kurahisisha usafirishaji wa mizigo, na kuimarisha miundombinu ya usafiri katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini.Pande zote mbili zilikubaliana kuwa ushirikiano kati ya bandari hizo unaweza Kuongeza kiwango cha biashara kati ya Tanzania na Msumbiji, Kurahisisha usafirishaji wa mizigo kupitia njia za bahari na nchi kavu, Kukuza uwekezaji katika sekta ya bandari na usafirishaji, Kuimarisha mahusiano ya kiuchumi na kidiplomasia kati ya mataifa hayo mawili,
Aidha, Balozi wa Tanzania alisisitiza umuhimu wa kubadilishana uzoefu wa kiutendaji, teknolojia za usimamizi wa bandari, pamoja na kuendeleza miradi ya pamoja inayoweza kuongeza ushirikiano wa bandari za ukanda huo.Kwa upande wake, Gavana wa Sofala alieleza dhamira ya serikali ya jimbo hilo kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuboresha miundombinu ya usafirishaji na kukuza nafasi ya Bandari ya Beira kama lango muhimu la biashara katika ukanda wa Kusini mwa Afrika.
Kikao kilihitimishwa kwa makubaliano ya kuendelea na mazungumzo ya kiufundi kati ya taasisi husika za bandari ili kubainisha maeneo mahsusi ya ushirikiano na hatua za utekelezaji.

